1. |
Nuun. Naapa kwa kalamu na yale wayaandikayo,
|
2. |
Kwa neema ya Mola wako Mlezi wewe si mwendawazimu.
|
3. |
Na kwa hakika wewe una malipo yasiyo katika.
|
4. |
Na hakika wewe una tabia tukufu.
|
5. |
Karibu utaona, na wao wataona,
|
6. |
Ni nani kati yenu aliye pandwa na wazimu.
|
7. |
Hakika Mola wako Mlezi ndiye Yeye ajuaye zaidi nani aliye ipotea Njia yake, na Yeye ndiye anaye wajua zaidi walio ongoka.
|
8. |
Basi usiwat'ii wanao kadhibisha.
|
9. |
Wanatamani lau unge lainisha ili nao wakulainishie.
|
10. |
Wala usimt'ii kila mwingi wa kuapa wa kudharauliwa,
|
11. |
Mtapitapi, apitaye akifitini,
|
12. |
Mwenye kuzuia kheri, dhaalimu, mwingi wa madhambi,
|
13. |
Mkavu, na juu ya hayo, mshari, amejipachika tu.
|
14. |
Ati kwa kuwa ana mali na watoto!
|
15. |
Anapo somewa Aya zetu, husema: Hizi ni simulizi za uwongo za watu wa zamani!
|
16. |
Tutamtia kovu juu ya pua yake.
|
17. |
Hakika tumewajaribu hawa kama tulivyo wajaribu wale wenye shamba, walipo apa kwamba watayavuna mazao yake itakapo kuwa asubuhi.
|
18. |
Wala hawakusema: Mungu akipenda!
|
19. |
Basi lilitokea tukio juu yake kutoka kwa Mola wako Mlezi, nao wamelala!
|
20. |
Likawa kama usiku wa giza.
|
21. |
Asubuhi wakaitana.
|
22. |
Ya kwamba nendeni kondeni mwenu ikiwa mnataka kuvuna.
|
23. |
Basi walikwenda na huku wakinong'onezana,
|
24. |
Ya kuwa leo hata masikini mmoja asikuingilieni.
|
25. |
Na walikwenda asubuhi, nao wameshikilia azimio hilo.
|
26. |
Basi walipo liona, wakasema: Hakika tumepotea!
|
27. |
Bali tumenyimwa!
|
28. |
Mbora wao akasema: Sikukwambieni, kwa nini hamumtakasi Mwenyezi Mungu?
|
29. |
Wakasema: Ametakasika Mola wetu Mlezi! Hakika sisi tulikuwa wenye kudhulumu.
|
30. |
Basi wakakabiliana kulaumiana wao kwa wao.
|
31. |
Wakasema: Ole wetu! Tulikuwa tumeikiuka mipaka!
|
32. |
Asaa Mola wetu Mlezi akatubadilishia lilio bora kuliko hili. Hakika sisi ni wenye kurejea kwa Mola wetu Mlezi.
|
33. |
Namna hivi yanakuwa mateso, na bila ya shaka mateso ya Akhera ni makubwa zaidi, laiti wangeli jua!
|
34. |
Hakika wachamngu watakuwa na Bustani za neema kwa Mola wao Mlezi.
|
35. |
Kwani tutawafanya Waislamu kama wakosefu?
|
36. |
Mna nini? Mnahukumu vipi?
|
37. |
Au mnacho kitabu ambacho ndani yake mnasoma?
|
38. |
Kuwa mtapata humo mnayo yapenda?
|
39. |
Au mnazo ahadi za viapo juu yetu za kufika Siku ya Kiyama ya kuwa hakika mtapata kila mnayo jihukumia?
|
40. |
Waulize: Ni nani miongoni mwao dhamini wa haya?
|
41. |
Au wanao washirika? Basi wawalete washirika wao wakiwa wanasema kweli.
|
42. |
Siku utakapo wekwa wazi mundi, na wataitwa kusujudu, lakini hawataweza,
|
43. |
Macho yao yatainama chini, fedheha itawafunika. Na hakika walikuwa wakiitwa wasujudu walipo kuwa wazima -
|
44. |
Basi niache na wanao kadhibisha maneno haya! Tutawavutia kidogo kidogo kwa mahali wasipo pajua.
|
45. |
Na ninawapururia muhula; hakika hila zangu ni imara.
|
46. |
Au unawaomba ujira, na wao wanaemewa na gharama hiyo?
|
47. |
Au iko kwao siri, basi wao wanaiandika?
|
48. |
Basi ingojee hukumu ya Mola wako Mlezi, wala usiwe kama mmezwa na samaki, alipo nadi naye kazongwa.
|
49. |
Kama isingeli mfikia neema kutoka kwa Mola wake Mlezi, bila ya shaka angeli tupwa ufukweni naye ni mwenye kulaumiwa.
|
50. |
Lakini Mola wake Mlezi alimteua na akamfanya miongoni mwa watu wema.
|
51. |
Na walio kufuru hukaribia kukutelezesha kwa macho yao, wanapo sikia mawaidha, na wanasema: Hakika yeye ni mwendawazimu.
|
52. |
Na hayakuwa haya, ila ni ukumbusho kwa walimwengu wote.
|