1. |
Naapa kwa wanao komoa kwa nguvu,
|
2. |
Na kwa wanao toa kwa upole,
|
3. |
Na wanao ogelea,
|
4. |
Wakishindana mbio,
|
5. |
Wakidabiri mambo.
|
6. |
Siku kitapo tetemeka cha kutetemeka,
|
7. |
Kifuate cha kufuatia.
|
8. |
Siku hiyo nyoyo zitapiga piga,
|
9. |
Macho yatainama chini.
|
10. |
Sasa wanasema: Ati kweli tutarudishwa kwenye hali ya kwanza?
|
11. |
Hata tukiwa mifupa iliyo bunguliwa?
|
12. |
Wanasema: Basi marejeo hayo ni yenye khasara!
|
13. |
Kwa hakika hayo ni ukelele mmoja tu,
|
14. |
Mara watakuwa kwenye uwanda wa mkutano!
|
15. |
Je! Imekufikia hadithi ya Musa?
|
16. |
Mola wake Mlezi alipo mwita katika bonde takatifu la T'uwaa, akamwambia:
|
17. |
Nenda kwa Firauni. Hakika yeye amezidi jeuri.
|
18. |
Umwambie: Je! Unapenda kujitakasa?
|
19. |
Nami nitakuongoa ufike kwa Mola wako Mlezi, upate kumcha.
|
20. |
Basi alimwonyesha Ishara kubwa.
|
21. |
Lakini aliikadhibisha na akaasi.
|
22. |
Kisha alirudi nyuma, akaingia kufanya juhudi.
|
23. |
Akakusanya watu akanadi.
|
24. |
Akasema: Mimi ndiye Mola wenu Mlezi mkuu kabisa.
|
25. |
Basi hapo Mwenyezi Mungu akamshika kumuadhibu kwa la mwisho na la mwanzo.
|
26. |
Kwa hakika katika haya yapo mazingatio kwa wanao ogopa.
|
27. |
Je! Ni vigumu zaidi kukuumbeni nyinyi au mbingu? Yeye ndiye aliye ijenga!
|
28. |
Akainua kimo chake, na akaitengeneza vizuri.
|
29. |
Na akautia giza usiku wake, na akautokeza mchana wake.
|
30. |
Na juu ya hivyo ameitandaza ardhi.
|
31. |
Akatoa ndani yake maji yake na malisho yake,
|
32. |
Na milima akaisimamisha,
|
33. |
Kwa nafuu yenu na mifugo yenu.
|
34. |
Basi itakapo fika hiyo balaa kubwa,
|
35. |
Siku ambayo mtu atakumbuka aliyo yafanya,
|
36. |
Na Jahannamu itadhihirishwa kwa mwenye kuona,
|
37. |
Basi ama yule aliye zidi ujeuri,
|
38. |
Na akakhiari maisha ya dunia,
|
39. |
Kwa hakika Jahannamu ndiyo makaazi yake!
|
40. |
Na ama yule anaye ogopa kusimamishwa mbele ya Mola wake Mlezi, na akajizuilia nafsi yake na matamanio,
|
41. |
Basi huyo, Pepo itakuwa ndiyo makaazi yake!
|
42. |
Wanakuuliza Saa (ya Kiyama) itakuwa lini?
|
43. |
Una nini wewe hata uitaje?
|
44. |
Kwa Mola wako Mlezi ndio mwisho wake.
|
45. |
Kwa hakika wewe ni mwonyaji tu kwa mwenye kuikhofu.
|
46. |
Ni kama kwamba wao siku watapo iona (hiyo Saa) hawakukaa ila jioni moja tu, au mchana wake.
|